AJTC VOICE FO VOICLESS

Ijumaa, 2 Desemba 2016

  MKEKA.jpg



Klabu ya Stand United ya Shinyanga imesema imechezwa na ‘machale’ ya kuwepo mchezo mchafu unaotaka kuchezwa na beki wao, Joseph Owino ambaye amekuwa akishinikiza apewe barua ya kuachwa, lakini ili kukwepa kesi wamemtaka aje na barua iliyosainiwa na hakimu ndipo wampe barua ya kumuacha ‘release letter’.

Owino hana maelewano mazuri na viongozi wake tangu abaniwe kujiunga na Fanja ya Oman ambayo ilikubaliwa kumchukua lakini ikashindwa kutimiza masharti ya Stand, ikiwemo kutuma kwanza fedha za kumununua kabla ya kupewa barua ya kumuacha lakini wakakataa.

Tangu kipindi hicho, Owino amekuwa kwenye msigano na uongozi wa Stand huku akibembeleza aachwe huru.

Katibu wa Stand, Kennedy Nyangi ameliambia Championi Ijumaa kuwa wamefikia wazo hilo kutokana na ukweli Owino anawadai fedha ya usajili, hivyo kumpa barua ya kumuacha ni njia ya kuwafungulia kesi.

“Siyo yeye tu, wachezaji wote waliosajiliwa msimu huu hakuna ambaye ameishapata fedha za usajili, lakini mwenyewe amezidi kutushinikiza tumpe barua ya kumuacha na kwamba atasamehe kila kitu.


“Tumemweleza kama amedhamiria kweli, basi atuandikie barua iliyosainiwa na hakimu kuthibitisha kwamba anaondoka kiroho safi, siyo tumpe barua halafu kesho atufungulie mashtaka, hilo hatutaki,” alisema Nyangi.

 

 

 



Hakika unaweza kushangazwa na namna Simba inavyohaha kuwabakiza vijana iliowalea na taarifa zinasema kijana aliyepewa unahodha, Jonas Mkude amewazimia simu viongozi wa klabu hiyo.

Habari za uhakika zinasema, Simba wamekuwa wakihaha kumpata Mkude ili kumalizana naye katika suala la usajili, lakini yeye alikuwa amezima simu tangu Jumatatu.

“Kweli Mkude alizima simu kabisa baada ya kuwa tumefanya naye majadiliano kwa mara ya kwanza. Kukawa hakuna mwafaka sahihi, wakati tunasubiri arudi kumalizana naye, akazima simu.

“Tulimtafuta kwa siku mbili, mwisho tukawaambia Meneja Mussa Mgosi na Mratibu, Abbas Ally kumtafuta. Nao wakafanya hivyo bila ya mafanikio na mwisho tumeamua kukaa kimya na kusubiri,” chanzo cha habari kutoka ndani ya Simba kilieleza.

“Sasa kama anataka kusaini sawa, au tumesikia kuna mtu kamshawishi asisaini ili akacheze Afrika Kusini sawa. Tunajua namna ya kulifanyia kazi hili na kupata jibu. Tumechoka kufanywa kama watoto.”

Imeelezwa, ili kuongeza mkataba Mkude alikuwa akitaka kupewa Sh milioni 80, baadaye akashuka hadi 60 wakati Simba walikuwa wameishia 40, wakapanda hadi 50 na Mkude ndiyo akaamua kuzima simu.

Wiki hii mwanzoni, Mkude aliliambia gazeti hili atakwenda kusaini Yanga badala ya Simba kama hali ya kutofikia mwafaka itaendelea.

Lakini siku chache baadaye, Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Clement Sanga naye akatoa kauli yake kwamba hawana mpango na Mkude na wanaangalia mbali zaidi kwa kusaka viungo ‘wakata umeme’ wenye uzoefu kwa ajili ya michuano ya kimataifa na inaelezwa hiyo inaweza ikawa sababu ya kumtia hofu Mkude na huenda akaanza kuwatafuta viongozi wa Simba, ili wamalizane.

Inaripotiwa kuwa juzi na jana Mkude alikuwa mmoja wa wachezaji wa Simba walioshiriki katika mazoezi ya timu hiyo kwenye Uwanja wa Chuo cha Polisi jijini Dar.
 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni